Alhamisi, Agosti 11, 2016

uNADHANI UNACHELEWA AU UMECHELEWA?

Somo: Unadhani unachelewa au umechelewa?


Mwl. Kelvin Kitaso, 0713804078

Watu wengi hushindwa kufurahia kwa kutokana na hali ya kudhania kuwa wanachelewa. Wengine wamekuwa na papara katika maisha na kufanya vitu visivyoeleweka kwa kudhania kuwa wanachelewa au wamechelewa. Uvumilivu ni kitu cha msingi sana na kitakusaidia kutokuwa na papara. Wengi wakiona marafiki zao wanamiliki magari wanajidhania wamechelewa na hulazimika hata kukopa mikopo ili tu na wao wanunue magari.
Nani kakuambia umechelewa, nan i kigezo gani kinakuonyesha unachelewa? Achana na hali hiyo na uanze kufanya mambo kwa utulivu na utaratibu.

Mambo Yanayoweza Kumkumba Mtu Anapojidhania Kuwa Amechelewa au Anachelewa.

·        Kufanya mambo kwa kukurupuka.
·         Kuishi kwa msongo wa mawazo, akili inakuwa haina utulivu.
·         Kusababisha gharama zisizo za msingi kwa sababu tu ya kukurupuka na kufanya vitu kwa pressure.
·         Kuanza kufanya mambo na kuishia katikati na kughairi tena kufanya.
·         Kukosa msimamo, na maamuzi mengi hufanya kulingana na upepo wa wakati huo unavyoenda.
·         Kuvutwa na upepo wa kila jipya linaloingia. Hapa ndipo unakuta mtu kila kikundi kikianzishwa yeye humkosi, kila biashara ikiingia utamkuta anajaribu, biashara za mitandao zimekuwa nyingi ila kila zikiingia yeye anajiunga kwa sababu anadhani amechelewa sasa anajitahidi kuwahi.
Wengine wanatafuta kazi sana na wanafika mahali wanaombwa rushwa ya fedha au ya ngono na hujikuta wanatoa kirahisi kwa kuwa wanadhani wamechelewa. Kumbe ungejizuia kutotoa rushwa kazi yako ingekuja tu kwa wakati wako, kujidhania kwako kuwa unachelewa ndiko kuna sababisha unapita njia ya mkato.
Wengi wanapita katika njia zisizo sahihi kwa kudhania kuwa wakipita katika njia zilizo halali wanachelewa, ila njia zisizo halali hazina Baraka. Ukweli ni kwamba bora ukawie kufika ila ufike salama kuliko kuwahi kufika ila si salama (yaani umefika tayari umetengeneza kovu). Njia za mkato kweli zinakufikisha kule unapotaka kufika ila si salama. Usijidhania kuwa umechelewa au unachelewa, wewe vumilia tu kupitia katika njia iliyo salama.
Nini ni alama ya kuchelewa kwako? Unaposema kuwa umechelewa kuoa au kuolewa nini ni alama inayoonyesha kuwa umechelewa au unawahi? Au unaposema umechelewa kupata kazi nini ni alama ya kuchelewa kwako ambayo ukiiangalia utasema ndiyo kiashiria cha kuchelewa kwako. Watu wengi katika maswali ya hapo juu utasikia wakijibu kuwa yaani marafiki zangu wote wameoa au wameshaolewa, au marafiki zangu niliosoma nao wote wameshapata kazi. Kipimo chako kikiwa ni wanadamu utaishi kwa kuteseka sana katika maisha haya. Kipimo chako mfanye kuwa ni Mungu. Maana ratiba za Mungu si sawa na wanadamu. Wanadamu wanaweza kusema kuwa ukiwa na miaka 23 unatakiwa uwe umeolewa na sasa una miaka 27 bado hujaolewa unajihisi kukata tamaa na kushuka kwa kuwa unadhani ulipaswa kuolewa ukiwa na miaka 23, hiyo ni kanuni za wanadamu tu ambao wao ufikiria hivyo ila inawezekana wewe umepangiwa kuolewa ukiwa na miaka 32. Kwa wanadamu umechelewa sana, ila katika ratiba za Mungu huo ndio wakati mwafaka.
Mungu hatakutendea jambo kwa kuwa kawaida za wanadamu zinasema hivyo, Mungu atakutendea kwa sababu wakati wake wa kukutendea umefika, na ndio maana kwa Mungu mwanamke wa miaka 90 anapata mimba, ila kwa sisi wanadamu mwanamke wa miaka 50 hawezi kupata mimba. Hii tafsiri yake ni kuwa muda wa Mungu si muda wa mwanadamu.
Unadhani Sara na Ibrahimu walichelewa kupata mtoto? Watu wengi huwa wanadhani kuwa Sara na Ibrahim walichelewa kupata mtoto kwa kuwa alipatikana wakiwa wazee sana. Ukweli ni kuwa kwa Mungu, Sara na Ibrahim hawakuwahi wala kuchelewa kupata mtoto ila walipata ndani ya wakati sahihi. Yaani wanadamu walikuwa wakiwashangaa ila ule ni wakati wa Mungu kwao. Hata wewe haujachelewa, wanadamu ndio wanakuaminisha uone kuwa umechelewa. Mungu ni Mungu wa majira na wakati.
Wanadamu sisi tunaamini kuwa mtu akimaliza tu chuo ndio wakati sahihi kwa Yeye kupata ajira, na mtu akikaa miaka 2 na kuendelea bila kazi tunasema kuwa amechelewa kupata kazi, na hata yeye huamini kuwa amechelewa na anachelewa kufanya maendeleo haswa anapowaona wenzie wakifanikiwa. Jambo la msingi kufahamu tena ni kuwa bado hujachelewa, Mungu anaratiba anayoijua juu yako.
Ukisoma katika kitabu cha Yeremia 29:11, Mungu anasema najua mawazo ninayowawazia, ni mema na wala si mabaya. Mara zote Mungu anayo mawazo yaliyomema, anayo ratiba iliyo njema maishani mwako na kwamwe hautachelewa.
“Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” Mhubiri 3:1
Katika biblia kuna habari za mwana mpotevu aliyemuomba baba yake ampe sehemu ya mali zake akafurahi nchi ya mbali, na aling’ang’aniza kupewa japo haukuwa wakati wake ila alikuwa na papara za kupata kwa wakati ule, alipopewa alienda kuzitumia vibaya na kufuja na mwisho wa siku alirudi akilia akiwa amechoka na hana hata kimoja katika vile alivyoondoka navyo kwa baba yake.
Usiwe na papara, fanya kwa sehemu yako kwa juhudi zote na umuachie Mungu akamilishe makusudi anayoyataka. Usimtangulie Mungu, mwache akutangulie.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni