Jumamosi, Julai 16, 2016

HILI NDIO TATIZO KUBWA AMBALO LINAPASWA KUPATA TIBA HARAKA ~Joas Yunus


Tunaishi katika dunia ambayo fikra hasi zimetawala .Watu wamekuwa karibu sana na fikra zao hasi kuliko uhalisia wa jambo.Fikra hasi umekuwa ugonjwa wa kuambukiza na sasa umeathiri sehemu kubwa ya maisha ya watu wengi sana duniani hasa vijana  na hivyo kupelekea ndoto zao kuyeyuka na sasa hawana tumaini la maisha yao ya kesho.

Watu wamekuwa wakiamini kila kinachoingia masikioni mwao bila hata kufanya mchujo wa nini kinafaa na kipi hakifai kwa mstakabali wa hatma ya maisha yao.

Wengi wameishi kwa historia za familia zao kwamba kamwe hawatafanikiwa na sasa wamekata tama maana hakuna aliyefika kubadilisha fikra zao.Watu wameishi katika kusadiki na kuamini katika yale waliyoaambiwa na waganga wa Kienyeji kuwa nyota zao zimechezewa .

Vijana wamejiingiza katika madawa ya kulevya kujiuza wenyewe kwa sababu ya fikra zao hasi  na kukataa tamaa ya kuishi .Hofu ya wasichokijua imekuwa kikwazo kikubwa na imepelekea vijana wengi kutodhubutu mambo mbalimbali ya kuleta maendeleo badala yake wamebaki wakilaumu ndugu zao na hata serikali kwamba haijawasaidia .

Fikra hasi zimewafanya vijana wengi kukaa bila kazi wakati wana uwezo na vipaji mbalimbali .Wamekuwa wakibagua kazi na kuchagua kazi zenye mishahara mikubwa na sasa umasikini na maisha magumu ndo wimbo wa kila siku kwao.

Dunia sasa imekuwa na vijana lukuki ambao hawana kitu cha kufanya lakini wakiwa na nguvu kubwa na uwezo mkubwa wa uzalishaji .Hali hii imekuwa mbaya zaidi  katika nchi zilizopo chini ya jangwa la sahara  na tatizo linaendelea kukua kwa kasi kila iitwapo leo.
Fikra hasi zimepofusha watu wengi na sasa wameshindwa kuona fursa mbalimbali zinazoweza kuwakwamua kutoka katika lindi la umaskini.

Vijana wengi wasomi wanatoka vyuoni na fikra hasi za kuajiriwa tena kwa mishahara mikubwa na badala yake wanakaa  muda mrefu wakitafuta hizo kazi za mishahara mikubwa na hawazioni na mwisho wanabaki kulalamika bila  kutafuta majibu  na sasa elimu yao imekuwa Elimu makaratasi na wengi wao sasa wameanza  kuitwa wasomi hewa .

Familia zetu zimekuwa zikijenga watoto katika mitazamo hasi bila kumfanya mtoto kuwa mbunifu na pengine kulea kipaji cha mtoto ambacho anaweza kukionesha wakati wa ukuaji .
Wazazi pia wamekuwa wakiwachagulia watoto masomo ya kusoma badala ya kuwaacha watoto kufuata ndoto zao .

Serikali na wadau hawajaweka mazingira wezishi kwa vijana kubadili mitazamo yao .Asasi za kidini pia zenye mchango mkubwa katika jamii hazijaweka mpango madhubuti wa namna ya kubadili mitazamo ya vijana na uwezeshwaji wa vijana juu ya tatizo hili.Matokeo yake kumekuwa na idadi kubwa ya vijana wenye mitazamo hasi  ndani ya asasi hizi .

Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam wakati akiwa Mkuu wa wilaya ya Kinondoni aliwahi kusema yafuatayo akiwa katika uzinduzi wa maonyesho ya tano ya Tanzania Homes Expo yaliyoandaliwa na Kampuni za EAG Group jijini Dar es Salaam. Tanzania ina rasilimali nyingi ambazo kama vijana  wangezitumia  zingeweza  kuwapatia ajira na  kuondokana  kukimbilia nchi jirani  kujihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya na kuishia kutofikia malengo yao. Fursa hizo zimekuwa zikichangamkiwa na wageni ambao wanatengeneza malighafi kwa kutumia rasilimali za hapa nchini.
Vijana wengi wanakimbilia nje ya nchi wanaziacha fursa na kushindwa kukuza uchumi wa nchi.


Kwanini vijana wengi wana mitazamo hasi??
  • Marafiki wabaya walio nao : vijana wameshindwa kujua kuwa maisha haya yanatokana na watu waliokuzunguka .Na kama unazungukwa na watu wenye mtazamo hasi basi hata wewe utakuwa hivo hivo .Vijana wengi sasa wameshindwa kuwa na jicho la tatu ya kujua nani na kwanini anapaswa kuwa rafiki yangu.
  •  Vitabu wanavyosoma: Kimuuingiacho mtu ndicho kimtokacho .Ni dhahiri kuwa vitu tunavosoma kwenye vitabu vina athari kubwa kwenye maisha yetu .Vijana wengi wamekuwa wasomaji wa vitu ambavyo haviwajengi .Vijana wengi hupenda vitabu vya mahusiano kuliko vitabu vya kuwaletea maendeleo yao na vinavyojenga maadili.
  • Vitu anavyosikiliza: Runinga zetu na radio zetu zina athari kubwa kwenye maisha yetu ya kila siku .Vijana wamekuwa wakisikiliza sana nyimbo za kuamsha mapenzi kwa muda mwingi badala ya kusikiliza vitu vya msingi vya kujenga maisha yao.
  • Mfumo wa Elimu yetu:Mfumo wa elimu pia umesababisha kuwajenga watu kuwa na mitazamo hasi ya kuamini kuajiriwa kuliko kutumia uwezo ulioko ndani ya mtu katika kuzalisha na kutengeneza ajira kwa wengine.
  • Mapokeo: Vijana wengi huamini katika kile walichokikuta katika familia zao ,nchi yao n.k. Huamini kuwa maisha ni bahati na nyote jambo ambalo si sahihi .

KWA USHAURI NA MAWAZO  NITAFUTE KWA NAMBA HIZI 

 0753836463

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni