MALEZI YA MTOTO (SEHEMU YA PILI)
NAFASI
YA MZAZI
MWL. KELVIN KITASO
CHUKUA MUDA WA KUTOSHA KUSOMA JAPO NI REFU
Wazazi wengi wamekuwa
na imani kuwa kazi yao kubwa ni kuzaa, kwa kutimiza lile kusudi la Mungu la
kuzaa na kuongezeka na kusahau kuwa baada ya kuzaa na kuongezeka kuna kazi ya
ziada ambayo inapaswa kufanywa na wazazi kama watu waliopewa dhamana ya
kumiliki uzao wao. Mzazi yeyote ili kuwa
mzazi bora ni lazima aige ni kwa namna gani Mungu analea watoto wake kwa kuwa
Mungu ni Baba, ni vyema kwa kila mzazi kuangalia ni kwa namna gani Mungu kama
Baba anafanya mpaka watoto wake huwa na tabia njema ambayo haifanani kabisa na ya
watoto wengine.
Kitabu cha Isaya
48:17 “……..Mimi ni BWANA, Mungu wako,
nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”
Kitabu hiki cha Isaya Mungu anajitambulisha kwa watoto wake ni nafasi gani
aliyo nayo kama mwalimu na kama kiongozi mbele za watoto wake. Nafasi hizi
ndizo alizo nazo mzazi mbele ya wanae.
Zipo nafasi ambazo
anazo mzazi katika malezi ya mtoto nazo ni kama:
1.
KIONGOZI
Mzazi ni kiongozi
katika familia na chini yake anao wafuasi wake ambao uitwa watoto na viongozi hawa
uwa ni katika ngazi kuu mbili, yaani kiongozi mkuu (mwenyekiti) ambaye mara
zote huwa ni baba na msaidizi wake ambaye ni mama (katibu). Viongozi hawa ndio
wakuu ambao huanzisha taasisi yao na katika taasisi yao hupatikana watoto,
hakuna taasisi isiyo na maono, hivyo viongozi hawa uhusika kutoa mwelekeo kwa
wafuasi wao ni kwa namna gani taasisi yao inapaswa kuwa na washirika wa hiyo
taasisi wanapaswa kuweje. Kuna nyakati kiongozi huwa na demokrasia lakini kuna
wakati ulazimika kufanya maamuzi ya kidikteta kulingana na aina ya wakati
uliopo. Ndivyo ilivyo kwa wazazi kwa kuwa kuna wakati watakuwa na hali ya
demokrasia na kuna wakati watakuwa na hali ya udikteta ili kuhakikisha mambo
yanaenda vyema katika familia. Mzazi akifaulu kuelewa kiongozi hupaswa kuwaje
ni lazima atakuwa mtu wa tofauti kuwasaidia watoto wake kufanya vizuri.
Kiongozi
ni mtu anayejua njia, anatembea katika njia na kuonyesha njia kwa wafuasi
wake. Na ndiyo nafasi kuu waliyonayo wazazi katika familia kama kiongozi.
|
Kujua
njia
Kujua njia ni sehemu
ndogo tu, ila ni ya msingi sana kwa mzazi yeyote yule kuijua njia ipasayo
kupitiwa, na ni muhimu kufahamu kuwa kama kiongozi hajui njia ni rahisi sana
kuwapoteza watu wake na kuwafanya wakapotea njia. Yesu Kristo ni njia na kweli
na uzima, Yesu ambaye ni njia uitwa neno. Njia ni neno la Mungu. Maandiko
yanasema kuwa ‘kipofu hawezi kumuongoza kipofu mwenzake kwa kuwa watatumbukia
wote shimoni,’ watoto uwa kama vipofu na uhitaji kupata mtu wa kuwashika ili
wasiweze kutumbukia shimoni. Mzazi aliye kipofu ni lazima ataishia
kuwatumbukiza watoto wake katika shimo.
Yohana 3:16
inazungumzia juu ya Mungu ambaye ni kiongozi bora na kiongozi makini na katika uongozi wake anaona ni muhimu
kupata kiongozi wa kuongoza familia yake na anamtoa mwanae pekee ili kila
anaemwamini na kuwa chini ya uongozi wake hasipotee. Kupotea kwa watoto ni
matokeo pia ya kukosa viongozi bora na viongozi wanaoijua njia.
Laweza kuwa fumbo
kubwa kulifumbua juu ya kuijua njia ila kuijua njia katika sehemu hii umaanisha
kufahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Mungu kwako kwanza kama mzazi na kisha
kufahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Mungu kwa watoto wako na pia kuangalia
kuyafanya hayo yaliyo mapenzi ya Mungu; na pia kuijua njia ni kufahamu njia
ambayo itamsaidia mtoto kukua katika makuzi yaliyo mema na kufahamu nini kama
mzazi ufanye ili kuimalisha makuzi mema katika familia yako.
Ni vyema kufahamu
kuwa kiongozi/mzazi hana njia moja tu katika kumkuza mtoto bali huweza kutumia
njia mbalimbali kuhakikisha mtoto anakuwa katika makuzi yaliyo mema na salama
mbele za Mungu. Anaweza tumia njia ya kidemokrasia pale inapobidi na kutumia
njia ya kidikteta pale inapobidi, ila kutumia njia moja tu kwa kila jambo ni
makosa na ni kukosa kuijua njia kama kiongozi.
Hautoweza kuongoza
familia yako kama haujui njia kwa kuwa hasiyeijua njia ni kama kipofu na kipofu
hawezi kuongoza kipofu mwenzake. Ila ni vyema kujua kuwa njia njema ni neno la
Mungu, kwa kulisoma na kulitafakari kama mzazi na kuliweka ndani linakupa
ufahamu wa kuijua njia ili uweze kuwasaidia na wengine kuijua njia.
Zaburi 119:105 “Neno lako ni taa ya miguu yangu, ni
mwangaza wa njia zangu.” Ni kwa kulifahamu neno na kuliweka ndani ya moyo
ndipo kiongozi anaweza kuwaongoza na washirika wake wakaijua njia sahihi.
Nafasi ya mzazi
katika kuijua njia ni nafasi ya kutafuta yeye mwenyewe kujifunza ili aweze
kuwafundisha na watoto wake.
Kimtokacho
mtu ni kile kilichoujaza moyo wake, ni busara kwa mzazi kujaa neno la Mungu
ili kuwasaidia watoto wake na pia hauwezi kutoa kitu ambacho wewe mwenyewe
hauna ndani yako, ila waweza kutoa ulichonacho tu, wayapokeayo na kujifunza
kwako ni yale uliyonayo.
|
Kutembea
katika njia
Haiishii katika
kuijua njia ila inakwenda mbali zaidi katika kutembea katika hiyo njia, yaani
kuyafanya yale uyajuayo. Katika kutafuta kuyajua yapi ni sahihi na yapi si
sahihi ni vyema kwa kiongozi kuyatenda yale hayajuayo kuwa ni sahihi.
Maxwell
anasema kuwa, “wafuasi umwamini kiongozi na kumfuata kuliko vile
wanavyojiamini wao wenyewe,”
|
jambo hili ni vyema
sana kwa mzazi kama kiongozi kulifahamu kuwa mara nyingi watoto uwaamini wazazi
wao na kupenda kuwaiga hata kama hawako sahihi kwa kuamini kuwa kama yanafanywa
na wazazi wao haina shida kwa wao kuyafanya, hata ukiwauliza watajibu mbona
hata Baba/Mama anafanya.
Nimeshawahi kuhojiana
na watu wengi sana na wengine wakiwa wakubwa kabisa na ukiwaambia kwa nini
unafanya kitu Fulani wao utoa jibu kwa kusema, “hata wazazi wangu walifanya
hivi hivi.” Kazi ya mzazi ni kuishi katika njia iliyo sahihi ili watoto wake
wapate kuona na kujifunza kwa kuiga kutoka kwao.
Wengine wanasema
“fuata maneno yangu, usifuatishe matendo yangu,” msemo huu utumiwa na jamii ya
watu walioshindwa kufanya yale yaliyo mema na yawatokayo vinywani mwao. Baba
mmoja wa kiroho aliyewaongoza watu wengi aitwaye Paulo kwa ujasiri alisema,
“nifuateni mimi kama mimi navyomfuata Kristo” kwa maana nyingine yeye kama
mzazi alijua na kufahamu kuwa ni jukumu lake kutembea katika njia na akahimiza
watoto wake watembee katika njia kama yeye anavyotembea. Na pia mtume Paulo
anasema juu ya watu waongozoa kuwa waigwe mwenendo wao ulivyo mwema katika
Kristo, na waongozwao waangalie sana mwisho wawaongozao kwa vile wanavyoenenda.
Ni vyema sana kwa wazazi kufahamu njia na kutembea katika njia na kuwa makini
katika yale wasemayo yaendane na yale wayatendayo.
Wazazi wengi
wamekuwa na kasumba ya kuwakemea watoto wao wanapokosea na kuwapa vitisho
vikali kwa yale mabaya wanayokuwa wameyafanya, na wengine husema. “ukirudia
tena nitakuchapa,” ila watoto wanaporudia maneno hayo ya mzazi hayatekelezwi na
mara nyingi wazazi uishia kupiga kelele na kutoa vitisho tena na tena, hali hii
ya kushindwa kutembea katika maneno ayasemayo mzazi uwasababisha watoto
kuwazoea wazazi na kutoona uzito katika mambo wayasemayo ila jambo la msingi ni
kwa mzazi kutimiza kile alichokisema kwa kuwa itamsababisha aaminike katika
yale ayasemayo na kumtia hofu mtoto kila anapofanya kosa. Na si katika upande
huu tu wa adhabu bali hata upande wa ahadi njema umfanya aamini kuwa wewe ni
mtu makini na mtekelezaji wa yale uliyomuahidi.
Wazazi wangu
walitulea kwa namna ya kutufanya kuogopa sana kukosea na kuwa makini sana
katika mambo tuyafanyayo kwa sababu ya ule ukali waliokuwa nao pale tulipokuwa
tunafanya makosa, wakati Fulani mimi na kaka yangu tulifanya kosa na Mama
akatuambia kwa kuwa mmefanya hilo kosa leo hamtolala ndani, na alikuwa
akimaanisha sana katika adhabu aliyoadhimia na katika kuadhimia huko alifunga
mlango na sisi tulikuwa tumekaa muda mrefu nje, tukisubiri labda aweza fungua
ila hakufungua mpaka tukaamua kutembea usiku kwenda kulala kwa dada (binamu) yetu, kwa kupokea adhabu ya namna
hiyo ilitufanya tumuone mama kuwa ni mtu anayemaanisha sana na ilitupa kuwa
makini sana na kukosea tena. Na alipokuwa akitisha tena tulikuwa makini maana
tulijua atafanya.
Mfano wa Mungu kama
kioo cha wazazi akiahidi ni lazima atatenda, na akisema ni lazima atafanya na
hii ni sababu inayozidi kumfanya Baba yetu kuonekana ni Mungu amaanishaye.
Mtoto akikosea
usiache kumpa adhabu ili aogope kurudia tena, hii ndiyo staiki ya mtoto na ndiyo
njia bora ya kumkuza mtoto.
Kuonyesha
njia
Kazi nyingine kubwa
na ya msingi sana kwa mzazi ni kuonyesha njia kama kiongozi kwa kuwa kiongozi
bora ni lazima aonyeshe njia kwa wale anaowaongoza, haishii kuijua njia ila
uzidi kwa kuionyesha njia kwa wale anaowaongoza. Kuonyesha njia ni kwema na ni
tendo ambalo si la siku moja au mwaka mmoja bali uwa ni tendo endelevu kwa
nyakati zote ambazo mzazi huwa pamoja na mtoto wake.

Kielelezo no:
1 Mfano wa picha ya mzazi akiwa
kiongozi kwa mwanae na mtoto kuvaa kama vile alivyovaa mzazi wake. Baba anaijua
njia, anatembea kwenye njia na anaonyesha njia. (Like a father, like a son)
Isaya 48:17 “……..Mimi ni BWANA, Mungu wako,
nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”
Mungu kama mzazi mkuu anaonyesha mambo yenye uwiano kwa kufundisha njia ili
upate faida na kuionyesha njia ipasayo, hii ni kusema kuwa yeye uhifahamu njia
ndiyo maana uionyesha lakini pia anatembea katika njia.
Namna
mzazi anavyoweza kuonyesha njia kwa mtoto akiwa kama kiongozi.
Ø Kwa matendo yako.
Kama mzazi ni muhimu
sana kuwa makini sana na matendo unayoyafanya kwa kuwa katika yale unayoyafanya
unaweza mjenga au kumbomoa mwanao/wanao. Maandiko yanasema kuwa, “alivyo mchungaji ndivyo walivyo watu
wake.” Watoto wao huwa na tabia ya kuiga sana na hupenda na wakati mwingine
hujisikia fahari sana kufanya yale ambayo hufanywa na wazazi wao, wengine
wakiwa katika michezo na marafiki zao huweza kurudia yote waliyoyaiga kwa
wazazi wao, kuwa makini kuijenga tabia ya watoto wako kwa kufanya yaliyo mazuri
machoni pao ili waweze kuiga yale yaliyo mazuri kutoka kwako kama kiongozi wao.
Katika matendo kuwa
makini sana na aina ya mavazi unayoyavaa kwa kuwa watoto pia hupenda kuiga
wazazi wao au watu wakubwa wanavaaje na ni mara chache sana wakaweza
kujisimamia katika maamuzi ya wavaaje, haswa kwa wale walio juu kuanzia miaka
12 na kuendelea. Kama mzazi unapenda kuvaa vimini/vinguo vifupi vifupi na
vyenye kubana, na vionyeshavyo baadhi ya maungo nje; ni rahisi sana kwa mtoto
wako kuiga hiyo tabia na kuanza kuvaa hovyo hovyo na kushindwa kujizuia katika
mavazi ayavaayo. Kiongozi anayevaa vibaya ni rahisi kwa wafuasi wake kuvaa
vibaya ila kwa kuvaa vizuri usababisha hata wafuasi wake kuvaa vyema.
Hauwezi kubadilisha
mtu kama wewe mwenyewe haujabadilika, kama mzazi ni mvaaji vibaya ni vyema
akabadilika kwa kuwa yeye ni muonyesha njia kwa kuvaa vibaya uonyesha njia ni
kwa namna gani watoto wake wanapaswa kuvaa. Si mavazi tu bali katika maeneo
mengi sana ya maisha mzazi ana nafasi kubwa ya kumsaidia au kumharibu mtoto kwa
matendo yake, kwa mfano vipindi vya redio, au television uviangaliavyo kama
muonyesha njia ndivyo unaweza mjenga au mharibu mtoto wako.
Kama muonyesha njia
jitahidi watoto wako wajue misimamo yako kama kiongozi wao na uwawekee mazingira
ya kuifuata misimamo yako kwa kuwa wewe ndiye mtoa dira ya ni kwa namna gani
wanapaswa kuwa.
David Oyedepo
anasema, “wazazi wanapaswa kuwaongoza watoto wao kwa wao wenyewe kuwa mfano kwa
matendo yao kwa kuwa watoto uiga sana kile kinachofanywa na wazazi wao.”
Ø
Kwa
maneno.
Ulimi ni kiungo
kidogo sana ambacho kinauwezo mkubwa wakuharibu na pia kinauwezo wa kujenga,
kwa ulimi wako kama mzazi waweza mjenga au kumharibu mtoto wako. Chiriku ni
aina ya ndege mwenye uwezo wa kuiga sauti ya mwanadamu kwa jinsi anavyoongea
japo hushindwa kutaja maneno katika kuiga huko. Ndivyo alivyo mtoto kwa kuwa ni
mtu ambaye hupenda kuiga sana maneno yanayosemwa na wazazi wake, wakubwa na
hata wadogo wenzake na ayasikiayo kwenye vyombo vya habari. Ni muhimu kwa mzazi
kuwa makini kwa maneno anayosema mbele za mtoto, na pia kumjengea mazingira ya
kutosikia maneno machafu yanayoweza kuharibu tabia njema.
Kwa nyakati za sasa
imekuwa ni kawaida kuona mtoto anatoa maneno mazito na mengine huwa machafu, na
ni kawaida sana kuona mtoto anashinda kijiweni na wakubwa na kutaniana nao na
kuwatukana matusi makubwa na wao kumtukana matusi makubwa pia, sababu kubwa ni
kuwa, watoto hupenda kuiga na katika kuiga kwao uathiriwa na aina ya yale
maneno wanayoyaiga.
1 Wakorinto 15:33 “Msidanganyike; Mazungumzo mabaya uharibu
tabia njema”. Mazungumzo mabaya yanaweza yakawa katika familia au nje ya
familia ila huwa na mchango mkubwa sana wa kuharibu tabia njema. Kama kiongozi
wa mtoto ni lazima uangalie kumsaidia mtoto kutosikia sikia maneno mabaya
ambayo yanaweza haribu tabia yake na hata akawa mtu mbaya.
Wapo wazazi ambao
hupenda kuwatamkia watoto wao maneno mabaya na ya kuwakatisha tamaa, kwa mfano,
wengine uwaita watoto wao ‘mbwa,’ ‘kenge,’ ‘nyau’, ‘chizi’, ‘mwehu’ na majina
mengi mabaya kwa sababu ya kuudhika na makosa ya watoto wao, na wengine
uwatamkia ‘sura mbaya’ au kuwakosoa katika baadhi ya maumbile yao kuwa ni
wabaya. Wakati wanayasema hayo wao uona ni kawaida sana ila kwa mtoto mambo
yale uenda ndani ya mioyo yao na wakati mwingine ujirudia rudia ndani yake na
kujiona kuwa hawana hata thamani kabisa kwa kule kufananishwa kwao na vitu
visivyo na thamani. Kuna wengine wameamua kuuza utu wao kulingana na kule
kutamkiwa kuwa ni wabaya na wenye maumbile mabaya na hawakuona thamani yao ndio
maana ikawa ni rahisi kwao kuuza utu wao na miili yao kwa kuwa kwao kitu cha kawaida na hakina thamani. Kwa
maneno ya namna hii wapo ambao ukumbuka hata katika ukubwa wao na kusumbuliwa
sana na maneno hayo hata ije neema ya Kristo iwatoe.
Katika jambo kama hili
ni muhimu sana kwa wazazi kuwa makini sana na vile wanawatamkia watoto wao kwa
kuwatamkia maneno mazuri, mazito na ya kuwatia moyo, ambayo yanawasababisha
kujiamini na kuwa watu watofauti hata mbele za wenzao. Watamkie Baraka na
mafanikio na maneno mazuri kwa kuwa yatasababisha kujiona wao ni watu wakubwa
na watofauti katika ulimwengu huu, wafanye waijue thamani yao na thamani ya
miili yao itawafanya waifunike vyema na kuiheshimu ili wengine waiheshimu na
kuiogopa. Maneno unayoyatamka yanawatengenezea kesho yao au katika utu uzima
wao watakuja kuwa watu wa namna gani, watamkie wao wakisikia na zaidi watamke
mbele za Mungu.
Ni wewe ndiye
unayeweza kuwafanya wajijue wao ni wakina nani na wanathamani gani katika
ulimwengu huu na miili yao ina thamani gani, kwa kufanya hivi utatengeneza
watoto wenye kujiheshimu sana na kujiheshimu kwa watoto ni utukufu na heshima
kwa wazazi na Mungu, ila kutojiheshimu kwao ni aibu kubwa kwa wazazi na hata
kumuaibisha Mungu aliyewaumba. Kwa mfano mtoto anayevaa vibaya na kuacha maungo
yake yapaswayo kufunikwa wazi ni sawa na kuwaweka wazi wazazi wake kwa kuwa
hata watu wanaponyooshea kidole utaja kuwa Yule ni mtoto wa Fulani, uzinzi na
kila aina ya uchafu aibu yake uenda kwa wazazi wake, mlee mtoto vyema aje
kukuletea heshima.
Nimeshawahi kuona
wazazi wanaofurahia watoto wao wanapozini, wanapopigana na watu
nakuwashinda(ugomvi), na mambo mengine kwa kuamini kuwa kwa kufanya hivyo ni
ujanja na kwenda na wakati na wengine wakiona wanavaa vibaya huona kuwa
wanaenda na wakati ila si kweli kwa kuwa kwa kufanya hivyo mtoto uingia katika
aina ya tabia ambayo si njema, na huweza kumfanya mtu kuharibikiwa na kupoteza
muelekeo wa maisha yake.
Ø Katika uchaguzi wa marafiki
Mtoto katika utoto
wake bado hutegemea sana uongozi wa wazazi wake katika uchaguzi wa marafiki kwa
kuwaelekeza kuchagua ni marafiki wa aina gani wanapaswa kushirikiana nao na
kuwa pamoja nao. Kuna umuhimu wa uhusika wa moja kwa moja wa wazazi kwa kuwa
katika hali ya utoto mtoto huweza kuambatana na chochote kile ila kwa muongozo
wa wazazi anaweza kujua ni yapi ya kuambatana nayo, na ni yapi ya kuachana
nayo.
Tabia ya watoto wote
ni kupenda kucheza na katika kucheza huko huweza kukutana na wenzake wenye
tabia mbalimbali na wakachangia kwa kiasi kikubwa kuharibu tabia njema
aliyotoka nayo nyumbani. Kama mzazi kuwa makini sana kuona mtoto wako
anashirikiana na marafiki wa aina gani akiwa nyumbani, shuleni, kanisani na
maeneo mengine mengi.
Usimzuie
kucheza kwa kuwa kucheza ni sehemu ya msingi sana kwa mtoto, ila muongoze katika
usahihi wa watu wa kucheza naye, mfanye kufahamu anapaswa kucheza na watu wa
aina gani.
|
Marafiki wabaya
uharibu tabia njema kwa yale wanayoweza kuzungumza naye, na hata yale afanyayo
mengi uchangiwa na marafiki. Angalia sana ni marafiki wa aina gani anaoshirikiana
nao na msaidie kukwepa kila aina ya marafiki isiyo na maana, marafiki wabaya ni
pamoja na wale walio na ushawishi mbaya juu yake na kuitetea dhambi na kuona ni
kitu cha kawaida sana na kutaka ionekane kama ni kitu cha kawaida kwa mwenzake.
Hofu ya Mungu ndani yao imepotea na uona mambo ya Mungu kama ni vitu vya
kawaida sana na hata akikosea hawawezi kumkosoa ila wanaweza kumtia moyo.
Kufahamu zaidi kuhusu mrafiki pata kitabu changu cha ‘huyu ndiye adui wa
mafanikio yako’.
2.
RAFIKI
Licha ya kuwa
kiongozi na mzazi kwake, mtengenezee nafasi ya kuwa rafiki yako ili uwe rafiki
wa karibu kuliko marafiki wote alionao katika maisha yake. Mfano wa kuigwa
ni Mungu, kwa kuwa yeye ni kiongozi,
mwalimu, mpaji, Baba (mzazi) ila mara zote uitafuta nafasi ya kuwa rafiki yetu.
Ukiwa rafiki kuna mambo atakushirikisha kwa kuwa U rafiki yake, na mambo hayo
kamwe hasinge kushirikisha kama ungekuwa mzazi tu, au kiongozi tu, au mkufunzi
tu. Watoto wengi wanapoanza kukua na kuingia katika ujana ukutana na mabadiliko
makubwa ya miili na viungo na katika mabadiliko hayo uwachanganya sana kwa kuwa
huja na uhitaji mkubwa wa kimwili na utafuta sana watu wa kuwashauri na
washauri wengine walio wengi uishia kuwashauri vibaya katika kukabiliana na
mabadiliko hayo na huwa ni sababu kubwa ya wengine kupotea wanapoingia katika
rika hili; utakopofanikiwa kuwa rafiki yake ataweza kukushirikisha na utapata
kumsaidia. Ila si wote ambao wanaweza kusema mpaka wachokozwe ila kuzingatia
jinsia ni busara kwa kijana wa kiume kuwa na baba na wa kike kuwa na mama.

Kielelezo no 2: Mfano wa baba na mtoto katika
urafiki, na kutoka pamoja.
Dr.
Mayle Munroe anapendekeza miongoni mwa njia njema ya kuwavuta karibu watoto ni
kufanya kama marafiki kwa kukaa nao chini na kuzungumza kuhusu maisha. Na kujua
vipi wanakwenda na mtazamo wao kuhusu maisha ni upi. Kila siku unayokaa na
watoto wako unawatengenezea kumbukumbu, sasa ni kumbukumbu za aina gani ambazo
unataka wawe nazo? Unataka watoto wako wakukumbuke vipi katika miaka ijayo;
kama mzazi anayeweza kucheka na kuchekeshana na kuwapenda wao kwa uwazi au
vinginevyo.”
3. MKUFUNZI
Licha ya kuwa
kiongozi na rafiki mbele za mtoto, mzazi pia ana nafasi kama mkufunzi au
mshauri. Katika harakati za kukua mtoto atakuwa anajipatia waalimu wengi sana
ila si kujipatia wazazi wengi maana wazazi ni wale wale na hauwezi
kuwabadilisha. Wazazi ndio walimu walio wakuu, yaani mwalimu mkuu na msaidizi
ni wazazi, na waalimu wengine wao huja kama walimu wakawaida tu. Kwa kuifahamu
nafasi hii ni vyema kwa mzazi kuwa makini sana kwa namna anavyoweza kumfundisha
mwanae ili awe salama.
Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye
hataiacha, hata atakapokuwa mzee”. Biblia inasisitiza katika kumlea mtoto
katika njia impasayo kwa kuwa hataiacha akikua, inapozungumza juu ya kumlea
inagusa maeneo ya kumfundisha, kwa kuwa ulezi ni pamoja na kumfundisha,
kumuelekeza, kumuonya, nakadharika.

Kielelezo no 3: Mfano wa mzazi kama mwalimu kwa watoto wake.
Ninapozungumzia
mwalimu sina maana ya kufanya kama wafanyavyo shuleni, japo hiyo inaweza kuwa
sehemu tu, ila maana yake kwa jumla na kwa mapana ni kumuelekeza juu ya yale
mema yote anayopaswa kuyafanya na kumpa elimu ili iwe uzima juu yake. Kujifunza
uambatana na mazoezi, majaribio kwa kufahamu kuwa yale umfundishayo kama yamemuingia.
Yapo maeneo mengi sana ya kujifunza kama, kupika, kufua, kuosha vyombo (kazi za
nyumbani), elimu ya kijinsia, na kazi nyingine nyingi za mikono, ila pia
kufundisha tabia njema kama kuheshimu wakubwa na kuwasalimia, kutii na
kuheshimu mamlaka yoyote iliyo juu yao, kuwa msikivu, kusaidia na kuwapenda
wengine na zaidi kumfundisha kweli yote iliyo ndani ya neno la Mungu.
Elimu ya namna hii
uchangiwa sana na wazazi kama watu wa karibu ya mtoto, hivyo mzazi ni vyema
kujiimarisha na kulitenda eneo hili kwa ufanisi mkubwa. Pia sehemu hii ina
uwiano mkubwa sana na ile sehemu ya uongozi kwa njia ya matendo kwa kuwa
mwalimu anapaswa pia kuambatanisha matendo yake na yale ayanayo yafundisha ili
iwe rahisi kwa watoto kuelewa somo.
Wekeza pia
mafundisho ya kutosha uwafundisha kuhusu elimu ya jinsia kwa kuwa wanasikia na
kuona mambo mengi kuhusu jinsia zao. Kumbuka wewe ni mwalimu mkuu ni lazima
usimame na wewe kumfundisha ni vipi anapaswa kuwa.
Kimtokacho mtu ni
kile kilichoujaza moyo wake na hauwezi kumpa mtu kile ambacho hauna ndani yako,
kama mwalimu kwa mtoto ni vyema kujaza yale yaliyo mema. Katika eneo la
ukufunzi mzazi uweza tumia njia mbalimbali ili kumfanya mtoto ajifunze.
4.
MHUDUMIAJI/MPAJI.
Nafasi nyingine ya
mzazi ni nafasi ya mpaji kwa mtoto wake na hii ni nafasi ya Mungu kwa watoto
wake kwa kuwa Mungu ni mpaji na mhudumiaji wa watoto wake. Katika nafasi hii ya
kuhudumia watoto, mzazi usimama kama mpaji kwa kuhakikisha anawapatia mahitaji
yote watoto wake wanayoyahitaji na ni jambo la msingi kwa mzazi kutoa ili mtoto
apokee.

Kielelezo no 4: mfano wa wazazi katika nafasi ya uhudumiaji,
akiwapatia watoto wake fedha.
Zipo huduma nyingi
ambazo mzazi anahusika moja kwa moja kumpatia mtoto na huduma hizo zipo katika
eneo la chakula, mavazi na makazi. Mbali na hapo mzazi uhusika kuhakikisha
anampatia mtoto elimu kwa kumsomesha na mahitaji mengine mengi ambayo uingia
katika haya.
Kama mzazi
atashindwa kumpatia mtoto wake mahitaji yake ni rahisi kwa mtoto kutafuta
wahudumiaji wengine ili wapate kumpatia mahitaji hayo, na wahudumu hao wanaweza
kumuathiri vibaya mtoto wako kwa kumpatia mahitaji yake kwa masharti ya
kumharibu kitabia na mwenendo.
Wakati Fulani kuna
msichana alikuja kwangu na kuanza kulalamika juu ya wazazi wake ambao wameacha
kufanya kazi yao ya upaji kwake, na katika kuzungumza nae alionyesha anauhitaji
mkubwa hata kuwa radhi kupata mwanaume anayeweza kumsaidia kupata mahitaji yake
na alijikuta anaingia kwenye mahusiano kutokana na uhitaji alionao. Ili ni
tatizo kubwa sana kwa walio wengi ni vyema kwa wazazi kujitahidi sana
kuwahudumia watoto wao vyema huku wakiwafundisha kuridhika na kuwa na kiasi, na
katika hili wazazi wazingatie kuwa na idadi ya watoto ambayo wataweza kuhimudu
na si kuzidisha ikaja kuwashinda katika kuihudumia.
Wazazi wanapaswa kulizingatia
sana swala hili, haswa kwa watoto wa kike ambao uwa na mahitaji mengi ambayo
utokana na jinsia yao, usiulize maswali mengi sana kwao haswa kwa wababa ndipo
umpatie, kwa kuwa kuna mambo mengine hawawezi kukuambia na kama hautotoa kwa
kuwa hawajakuelezea utawafanya kuwatafuta marafiki wakiume ambao
watawashirikisha ili wawe wakiwapatia mahitaji yao.
Mungu kama mpaji
mkuu aliye mfano wa wazazi anawaambia wanae kuwa, “ombeni nanyi mtapewa………. kwa
kuwa kila aombaye hupewa,” hii ni hatua njema kwa mzazi kuifikia japo si kila
jambo waweza mpatia aliombalo kwa kuwa akiomba lisilo jema si rahisi kumpatia
na pia kuna mengine yapo nje ya uwezo wako kuyatoa ila ni muhimu kufahamu kuwa
ukiombwa ni vyema kutoa kwa kuwa ni mpaji kwake ila tu kama yapo ndani ya uwezo
wako.
Kiongozi mmoja wa
kiroho alishuhudia kwa namna anavyosimama katika nafasi hii ya upaji kwa watoto
wake na kusema ni kwa namna gani utoa mahitaji ya watoto wake pale wamuombapo
na afanyapo hivyo hujisikia vizuri kwa kutimiza wajibu wake kwa watoto wake na
hutiwa nguvu zaidi anaposikia neno ‘ahsante’ kutoka kwa wapokeaji wake na humpa
nguvu ili kufanya zaidi na zaidi. Neno ahsante si kwa wazazi wa kimwili tu hata
kwa Mungu aliye mbinguni hupenda sana watoto wake wanaposema ahsante pale
anapotoa mahitaji kwao.
Katika kutoa huduma
mzazi ni lazima kuangalia na kukwepa sana kuwa na upendeleo kwa watoto ila kwa
watoto wa kike ni vyema sana kupewa vipaumbele vya utofauti kulingana na
mahitaji yao kuwa ni mengi ukilinganisha na walivyo watoto wa kiume, ukaribu na
huduma njema kwao ni ulinzi wa kutoharibikiwa.
Kuna hadithi ya
zamani ya kaka ‘M’ alimpatia zawadi rafiki yake ‘S’ na alirudia zaidi ya mara
moja na wakati mwingine alimpatia zawadi ya aina ile ile tena, ‘S’ alipoipokea
akaiangalia na hakusema neno ahsante bali alianza kumlaumu kwa nini amemletea
ya aina ile ile, ‘M’ alitulia kimya pasipo kujibu lolote, akawaza kuwa, kwa
nini nilimpa yeye ni bora ningempa mtu mwingine angesema ahsante, tangu wakati
ule moyo wake uliingia uzito sana kumpatia ‘S’ kitu chochote, ila kuna mwingine
alifanyiwa kitu kidogo sana na ‘M’ alishukuru sana mpaka akamwambia Mama yake,
kwake ilimpa nguvu kumthamini huyu wa pili kuliko Yule wa kwanza, Mfano huu ni
vyema kujifunza kwao kwa kuwa ndivyo Mungu anavyotuchukulia na sisi kwa tabia
zetu za kushukuru.
Ni jambo la busara
kwa mzazi kumfundisha mwanae/wanawe kuwa na shukurani kwa chochote wakipokeacho
kwa kuwa ni vyema kwa mtoto kuwa na shukurani kwa kila apokeacho kutoka kwa
wazazi wake na watu wengineo, kwa kusema ahsante anasababisha wazazi wake
wapate nguvu ya kumuhudumia zaidi, kwa chakula wampatiacho, mavazi wampatiayo,
elimu wampatiayo, na mahitaji mengi watoayo kwake ni busara na hupendeza sana
kwa mtoto kusema ahsante. Neno asante humtia nguvu sana alipokeaye kutenda zaidi
na zaidi. Hakuna mzazi anayependa mtoto asiye na shukurani ila wazazi wote
hufurahishwa na neno ahsante.
Katika kupokea ni
vyema pia kwa mtoto kuwa radhi na tabia ya kuridhika na kupokea kwa shukurani
yale ayapokeayo kutoka kwa wazazi wake. Kuifahamu hali ya wazazi ni vyema sana
na kutamfanya mtoto kuwa radhi na kile kinachopatikana.
5.
MPANZI
Mzazi ni kama mpanzi
na mtoto ni sawa na udongo, neno la Mungu ni mbegu ipandwayo. Inategemea mzazi
amebeba mbegu(neno) kwa wingi gani ili aweze kupanda katika udongo alionao.
Neno la Mungu usema kuwa “neno la Kristo
likae kwa wingi ndani yenu, kolosai 3:16,” Mzazi ni lazima ahakikishe
amebeba neno(mbegu) za kutosha ndani yake ili kupanda na ni lazima awe makini
kulitunza shamba lake kwa umakini mkubwa ili aje kupata kile alichokipanda.
Kama ilivyo kwa
mpanzi uwa makini kupambana na wadudu na wanyama wote watakao kuharibu mazao
yake, ndivyo impasavyo mzazi kuwa ili kulinda shamba lake.
Wagalatia “Msidanganyike; apandacho mtu, ndicho
atavuna,” kamunapanda neno ni lazima utavuna matokeo ya lile neno ulilolipanda
na ukipanda mambo ya ulimwengu huu kwa mwanao ni lazima yatakurudia hayo
uliyoyapanda tena kwa wingi kwa kuwa mbegu moja ya mahindi uzalisha mahindi
mengi sana. Naye lazima atazidi zaidi ya kile alichokipokea.
6.
MFINYANZI
Pia mzazi ni
mfinyanzi na mtoto ni udongo, kama mfinyanzi ubeba picha ya mtoto anapaswa
kufananaje na ujishughulisha kuhakikisha kuwa mtoto afinywangaye yupo katika
hali njema na ya kulidhisha. Mtoto uwa kwa vile umfinyangavyo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni