JIFUNZE KWA WALIOKUTANGULIA
By, Kelvin Kitaso….
0713804078, 0769190019
“Kikomo cha
mwenye hekima katika kujifunza ni siku anayokufa, lakini mpumbavu hukinai
kujifunza yungali anaishi”
Katika maisha
kujifunza ni kitu muhimu sana na endelevu, kujifunza si ujinga ila ujinga ni
kushindwa kujifunza. Wengi hudhania kuwa kujifunza ni kuingia darasani tu, ila
kujifunza si kuingia darasani na ni zaidi ya kuingia darasani. Kwa sababu mtu
anaweza akawa darasani halafu asifanikiwe kujifunza na mwingine akawa nje ya
darasa akajifunza vizuri zaidi.
Wengi hushindwa
kufanya mambo ya msingi yanayoweza kuwasaidia kutoka katika maisha yao kwa
sababu ni wavivu kujifunza.
Usionee mtu aibu
ya kujifunza hata kama unamzidi umri, mali, fedha, elimu ila kama kuna taarifa
anazifahamu kuliko wewe jishushe na ukubali kujifunza kutoka kwake.
“Uvivu wa kujifunza ni chanzo cha ujinga”
Kabla hujaanza
kufanya jambo unalohitaji kulianza anza kwa kuwauliza waliokutangulia
walifanyaje au wanasemaje juu ya jambo kama hilo, na uliza wengi kwa kadiri
uwezavyo hiyo itakufanya kupata taarifa nyingi ambazo zitakufanya kuwa bora
zaidi yao na kutakufanya kupunguza wingi wa vikwazo ambavyo ilikuwa ukutane
navyo.
Jifunze katika
vitabu maana humo kuna taarifa nyingi zimekusanywa, kwa kadiri unavyosoma
ndivyo unazidi kupata maarifa yatakayo kusaidia kuyaboresha maisha yako.
Kabla hujaingia
kwenye ndoa anza kujifunza kuuliza waliopo kwenye ndoa, soma vitabu ambavyo
vitakufanya uwe na taarifa na maisha ya ndoa yapoje, kaa chini na wazazi au
walezi wako jifunze kwao na uliza maswali mengi kwa kadiri uwezavyo. Kumbuka
kujidhania kuwa unajua sana kutakusababisha kuja kushindwa vibaya sana.
Siku moja nikiwa
na rafiki yangu tukibadilishana mawazo kuhusu uzoefu wa maisha ya ndoa katika
uzuri na changamoto zake, tukaanza kuzungumzia changamoto ya mwanandoa kutoka
nje ya ndoa, kisha akaniuliza kama itanitokea mimi nimejiandaa kukabiliana nayo
kwa namna gani? Niliposikia swali hilo nikacheka sana na kicheko kilipokatika
nikaingiwa na huzuni na kujihurumia kwa kuwa sikuwahi kuwaza changamoto kama
hiyo. Si vitu vizuri kuvizungumza ila ukijifunza mapema lolote litakapokukuta
halitokusumbua.
“Kujidhania unajua si kujua”
Kabla haujaanza
biashara, kampuni au kiwanda tumia muda mwingi kujifunza sasa maana kuna siku
utatamani kujifunza hautopata muda wa kufanya hivyo, jifunze kwa wanaomiliki
viwanda wanafanyaje, wanaendeshaje maisha yao, na kila kitu kinachohusu
uzalishaji, usambazaji, masoko, kodi, n.k.
Kabla hauja anza
kilimo au ufugaji jipe muda wa kujifunza vya kutosha yahusuyo kilimo au ufugaji
katika uzuri na changamoto zake.
Unapoamua
kujifunza kitu usiegeme upande mmoja, tafuta kufahamu uzuri na ubaya wa hiko
kitu, na ujiandae kukabiliana na huo ubaya kwa namna ya kuushinda.
Katika kujifunza
uliza swali lolote kwa mtu ambaye anajua zaidi yako maana kuuliza si ujinga na
usione aibu maana umekusudia kujifunza. Acha kuitii sauti inayosema sijui
atanielewaje, wewe angalia kuwa unapaswa kujifunza.
Katika kujifunza
usiangalie mtu, angalia kitu unachotakiwa kujifunza kwa huyo mtu.
Unapoingia
sehemu usijifanye wewe unajua zaidi ya wote na ukaanza kupiga kelele na kuongea
unayofanya hiyo itakupa ufinyu wa kujifunza, ukifika sehemu kaa kimya kwanza
uwasikilize wengine wana nini na wanafanya nini ili upate kujifunza. Penda
kusikiliza yaw engine zaidi ya unavyopenda watu wasikilize ya kwako.
Usijidhanie
kwamba umejitosheleza, kila siku unapoamka jua kuna kitu kipya unapaswa
kujifunza, kaa tulia na ujifunze kwa kusoma, kusikiliza audio, kuangalia DVD,
au kwa kuzungumza na kusikiliza kwa wengine. Kama usipoiweka akili yako katika
mfumo wa kujifunza hata somo jipya likija hautojua kama unapaswa kujifunza.
Msemo huu ni
msemo wa ujinga na upumbavu. Unaposema si wasomaji wa vitabu maanaake si
watafutaji wa maarifa na mtu asiye na maarifa ni mjinga na anayekataa maarifa
ni mpumbavu.
Kunatofauti kati
ya mjinga na mpumbavu, mjinga ni mtu asiye na maarifa (hajui/hana ufahamu) ila
akipata hayo maarifa hatokuwa mjinga tena.
Mpumbavu ni mtu
anayekataa maarifa, yaani anajua kabisa haya ni maarifa na yanasaidia ila yeye
hataki.Vitabu ni
maarifa ambayo hujenga nafsi, na nafsi ndipo kuna mfumo mzima wa maisha ya
mwanadamu yaani mfumo wa utajiri na hata umaskini vyote vyaweza kutokea huko
kulingana na aina ya taarifa unazoingiza.
Ukitafsiri sasa
ule msemo uliozoewa sana utagundua tafsiri yake ni Waafrika ni wapumbavu (watu
wasiotaka maarifa). Msemo huu una ukweli kwa sehemu yake kwa kuwa waafrika
wengi hawapendi kujifunza na hata wale wanaoitwa wasomi, usomi wao umeishia
katika yale wanayofundishwa darasani tu. Siri kubwa ya kufanikiwa ipo katika
kuyapata maarifa na maarifa huja kwa kujifunza na kujifunza huja kwa kusoma,
kusikiliza na hata kuona.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni