Jumanne, Septemba 13, 2016

         UNYOPASWA KUYAFAHAMU KUHUSIANA NA SADAKA YA LIMBUKO

Hii ni sadaka ambayo ni ya mwanzo wa kila pato ulipatalo katika yale uyafanyayo. Kama ni biashara basi yale mapato ya kwanza ni malimbuko yako kwa BWANA, kama ni kazi huwa mshahara wa kwanza, kama ni mazao huwa yale ya kwanza na vivyo hivyo kwa wanyama. Sadaka hii pia kwa nyakati za leo huwasilishwa kanisani.

Ezekiel 44:30 “Na kitu cha kwanza cha malimbuko yote ya vitu vyote, na kila toleo la kila kitu cha matoleo yenu, litakuwa la makuhani. Tena mtampa kuhani sehemu ya kwanza ya unga mbichi, ili kukalisha Baraka juu ya nyumba yako.

Mithali 3:9:10 “Mheshimu BWANA kwa mali yako. Na kwa malimbuko ya mazao yako yote. 10 Ndipo ghala zako zitakapojazwa kwa wingi, Na mashinikizo yako yatafurika kwa divai mpya.”

Kuna umuhimu mkubwa sana wa kutoa malimbuko, na ukweli ni kuwa hii sadaka ni sadaka ambayo haina kipaumbele kwa watu. Wengi hawafahamu kabisa kuhusu hii sadaka na hata wanaofahamu ni wachache sana wanaoishiriki ipasavyo.

Ukisoma maandiko hapo juu utaona kuna Baraka nyingi sana zinatajwa kuambatana na mtu anayetoa malimbuko. Kwenye kitabu cha Ezekiel anasema Baraka zitakaa juu ya nyumba ya huyo mtu. Kuna tofauti kubwa ya Baraka kukaa na kuja, zinaweza kuja na kuondoka lakini zikikaa hudumu mahali hapo hapo bila kuondoka. Maanaake nyuma ya mtu anayetoa malimbuko si nyumba ya kawaida, ni nyumba iliyojaa Baraka na kila kilichomo ndani yake kimebarikiwa na kila kizaliwacho ndani ya hiyo nyumba kimebarikiwa pia, na hata mgeni akiingia kwenye hiyo nyumba ni lazima abarikiwe. Malimbuko yanavuta Baraka za Mungu kuishi na mtu.

Mtu ambaye kazi yake anaitolea malimbuko hakuna adui anayeweza kuigusa na kufanya chochote kile anachohitaji kukifanya. Mtu wa namna hii kuna kuinuliwa ‘promotion’ nyingi zitakuwa zinafanyika kwa ajili yake.

“kama mazao/mapato yako ya kwanza yamebarikiwa basi lazima vyote vinavyokuja baada ya hayo view vimebarikiwa”

Watu wengi huwa hawaelewi kuwa sadaka huwa zinadai Baraka mbele ya madhabau ya Mungu na ndio maana anayetoa sadaka kwa uaminifu mbele za Mungu maisha yake mara zote siyo maisha ya kawaida.

Dr. Michael Hutton-Wood anaelezea uzoefu wake katika malimbuko kuwa tangu Mungu amemfunulia siri ya kuelewa nguvu ya malimbuko akaamua kuinuka na kutembea katika kanuni ya kutii na kutoa. Yeye kila anapoanza mwaka, mapato yote ya mwezi January lazima ayatoe mbele za Mungu, na ikiwa mapato yake ya kwanza yamekuwa matakatifu mbele za Mungu basi mapato yote yatakayokuja baada ya hapo yatakuwa yamebarikiwa.

Napenda kubarikiwa, kumiliki vitu vizuri kwangu haitoshi, nataka kumiliki vitu vizuri huku nikiwa ndani ya mfumo wa Baraka za Mungu. Namshukuru Mungu kwa kuifunua siri hii katika maisha yangu.

Ukweli ni kuwa mwezi Januari haswa kwenye jamii zetu za Kiswahili huwa maarufu kama mwezi mgumu kifedha kwa kuwa watu wanakuwa wametoka katika msimu wa sikukuu za Christmas na mwaka mpya lakini pia huwa na majukumu ya kupeleka watoto shule haswa kwa wale wenye familia, inakuwa ngumu kumwelezea mtu asiyejua maana ya sadaka kuwa anapaswa kutoa pato lake ili kutakasa mapato yake ya mwaka mzima. Ila sijawahi kumuona mwenye haki ameachwa kwa sababu ya haki yake.

Hata kama umeangaika kupata kazi muda mrefu na imetokea umepata halafu unamadeni mengi usikulupuke kuanza kula hela ya Mungu. Tulia na uipeleke mbele za Mungu (soma tena Ezekiel 44:30), unapoipeleka mbele za Mungu unasababisha Mungu awe anaiangalia kazi yako kwa umakini, atailinda kazi yako, hata kama kuna watu wanataka kuipoteza haki yako ya kufanyiwa promotion hawatakuwa wanapambana nawe bali watakuwa wanapambana na Mungu mwenyewe na utapewa hata hekima ya kutumia mshahara wako ili isiwe kama wale walioweka fedha zao katika mifuko iliyotoboka toboka.

Hagai 1:6 “Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hakuna aonaye moto; na yeye apateye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka.”

Bila shaka umeshawahi kukutana na mtu anakwambia toka aanze kufanya kazi haoni faida yake, hata mshahara anaoupata haujawahi kufanya kitu chochote cha maana. Siri imejificha humu katika utoaji. Maana Mungu anasema atamkemea yeye alaye ila kama tukitoa zaka na dhabihu, sasa atakemewaje yeye alaye kama mtu hatoi?


Mungu anaheshimu sana pale unapoamua umuheshimu kwa kile ulichonacho na ndio maana kwenye Mithali 3:9-10 anasema akiheshimiwa kwa malimbuko yetu ni lazima ghala zetu zijazwe kwa wingi na kufikia viwango vya kufurika.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni