FANYA BIDHAA YAKO KUWA BORA ZAIDI.
Dunia hii watu wanaofanya vitu kama unavyofanya wewe ni wengi sana na wanazaliwa kila siku, ila kitu pekee kitakachokutofautisha na hao wengi ni ubora tu.
kuna wahubiri wengi sana ila wanaosifika na kupendwa sana ni wachache, kuna waimbaji wengi ila wanaosifika na kupendwa ni wachache sana, kuna waandishi wengi ila wanaosomwa ni wachache kulinganisha na wingi wa waandishi.
Hakuna kitu kipya utakachotuletea utuambie kuwa ni kitu kipya... hakuna jipya chini ya jua. vyote hivyo unavyoviona vilikuwepo tangu zamani, kazi yetu ni kuviboresha tuvifanyapo na kuvifanya kuwa bora zaidi.
Wakati nimemaliza kitabu changu cha kwanza nilichoanza nacho cha "uungu wa mwanadamu" nilimfuata bishop mmoja na kumuelezea maudhui ya kitabu kile kuwa nina kitabu nimeandika vitu kama vipya maana sijasikia mahali popote nilitulia tu katika kutafakari na Mungu akanipa hiyo!! yule bishop akacheka na kuniambia mbona hakuna kitu kipya yaani ni lazima kutakuwa na wengi tu waliofundisha kuhusu hiko kitu. wakati ule nalikuwa mgeni sana na mitandao na nilikuwa sifahamu mambo mengi sana ukilinganisha na sasa japo kwa sasa pia bado mengi tu sijayafahamu. baada ya miezi kadhaa naliitwa kahama kwenda kufanya huduma, nalipokuwa huko nalikuta kitabu cha Bishop Oyedepo, nilipoanza kukisoma nalikutana na yale mambo niliyoyaandika na ufahamu ukanijia zaidi kuwa yale wewe uyaonayo mapya na kujidhania pengine ni wewe tu unayajua kumbe wapo wanaojua hayo hayo hata zaidi ya vile wewe unayajua.
usiridhike na hiko ulichonacho leo, tafuta kila njia ya kuongeza ubora siku hata siku.
Mwimbaji mmoja alinitafuta na kunieleza kuwa anahitaji kutoa albamu yake ya nyimbo saba hivi, nikamwambia naomba nitumie nisikilize kabla ya kwenda studio japo sina utashi wa uimbaji ila kizuri na kibaya nakielewa tu. niliposikiliza zile nyimbo hazikunipendeza kabisa nikamwambia msaada mkubwa wa kwanza naweza kufanya ni kumpatia mwalimu mwenye uzoefu mkubwa amnoe kabla ya studio. nilipomuunganisha nae wakawa hawaelewani na mwimbaji yule alijiamini kuwa anajua na nyimbo zake zilipofikia hazihitaji kufanyiwa hayo marekebisho. Hapo ndipo tuliponyoosha mikono maana kumfundisha mtu anayejua ni kazi sana.
usiweke chuki wala uhasama na watu waliobora, jisogeze karibu nao hata kwa gharama yoyote ili ikusaidie kuwa bora.
Bora uchelewe kufika lakini ukafika salama kuliko kuwahi kufika huku umepata majeraha.
Mambo mazuri hayahitaji haraka/papara
Hiyo albamu unayoipeleka haraka haraka ili tu itoke 2016 ni bora ungejipa muda wa kutosha ili hata ikitoka 2017 iwe bora zaidi ya sasa.
Hiko kitabu unachokipeleka mbio mbio ili tu kitoke sasa ni bora ungevuta muda kuandaa bidhaa iliyobora zaidi.
Si unafahamu kuwa vitu visivyobora huwa vinaboa.
usifanye vitu kwa kisingizio cha kuwa unakimbizana na muda. Acha kushindana na muda, hakuna aliyewahi kukimbizana na muda akaushinda.
Jipe muda, fanya kwa ubora, hakiki kazi zako mara kwa mara ili utakapokuja kufanya chochote kila mtu avutiwe na kile ulichokifanya.